Mashindano ya CAF ya msimu wa 2024/25 yanatarajiwa kuwa mtihani mkubwa kwa vigogo viwili vya soka vya Tanzania, Young Africans (Yanga) na Simba SC. Baada ya droo za hatua ya makundi za Ligi ya Mabingwa wa CAF na Kombe la Shirikisho la CAF kuchezwa, mashabiki wa soka nchini Tanzania wanasubiri kwa hamu kuona jinsi vilabu vyao vitakavyofanya dhidi ya timu bora zaidi katika bara la Afrika.
Young Africans kwenye Ligi ya Mabingwa wa CAF
Mabingwa watetezi wa ligi ya Tanzania, Young Africans, wamepangwa kwenye Kundi A la Ligi ya Mabingwa wa CAF wakiwa na wapinzani kama mabingwa mara tano wa mashindano hayo TP Mazembe kutoka DR Congo, vigogo wa Sudan Al Hilal, na MC Alger kutoka Algeria. Yanga italazimika kuonyesha kiwango bora sana ili kufanikiwa kupita kwenye kundi hili gumu.
Baada ya mafanikio ya hivi karibuni ya ndani na kwenye mashindano ya kimataifa, Yanga si wageni kwenye mashindano haya. Wameonesha ubora katika misimu michache iliyopita na kujitambulisha kama timu hatari zaidi kutoka katika ukanda huu wa CECAFA na sasa watakuwa wakitafuta kufanya vizuri zaidi katika kampeni hii.
Kundi A la Ligi ya Mabingwa wa CAF:
TP Mazembe (DR Congo)
Young Africans (Tanzania)
Al Hilal (Sudan)
MC Alger (Algeria)
![]() |
Makundi yote ya Klabu Bingwa Afrika 2024-2025 |
Simba SC kwenye Kombe la Shirikisho la CAF
Kigogo mwingine wa soka la Tanzania, Simba SC, watashiriki katika Kombe la Shirikisho la CAF baada ya kukosa kufuzu Ligi ya Mabingwa mara baada ya kumaliza ligi ya ndani wakiwa nafasi ya tatu nyuma ya Yanga na Azam, Wamepangwa katika Kundi A la Kombe la Shirikisho ambapo watakutana na CS Sfaxien kutoka Tunisia, CS Constantine kutoka Algeria, na Bravos do Maquis ya Angola.
Kundi hili linaonyesha changamoto kubwa kwa Simba, lakini tayari wamejidhihirisha kuwa na uwezo wa kufanya vizuri katika mashindano ya kimataifa misimu iliyopita. Wakiwa na kikosi imara na uongozi wenye uzoefu, Simba watajitahidi kufika mbali kwenye mashindano haya na kuleta heshima kwa soka la Tanzania.
Kundi A la Kombe la Shirikisho la CAF:
Simba SC (Tanzania)
CS Sfaxien (Tunisia)
CS Constantine (Algeria)
Bravos do Maquis (Angola)
Nyakati za Kusisimua kwa Soka la Tanzania
Yanga na Simba zote ziko tayari kujitwika majukumu katika mashindano yao. Baada ya droo kukamilika, sasa mkazo unahamia kwenye maandalizi ya hatua ya makundi, ambayo yataanza mwishoni mwa mwezi Novemba. Mashabiki wa soka wa Tanzania watakuwa nyuma ya timu zao wakitarajia mafanikio na kuona jinsi watakavyowakilisha nchi kwenye mashindano makubwa ya soka la Afrika.
Na Luck Mwaifuge
Post a Comment